JKCI NDANI YA SOKO KUU LA KARIAKOO, WANANCHI KUPATA HUDUMA BURE NDANI YA WIKI MOJA
Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) imefungua rasmi kliniki ya uchunguzi na matibabu katika Soko Kuu la Kariakoo kwa ajili ya kuwahudumia wafanyabiashara, wananchi wa eneo la Kariakoo ikiwemo wateja wanaofika sokoni hapo kutoka nje na ndani ya nchi.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa Kliniki hiyo Meneja Mkuu wa Shirika la Masoko ya Kariakoo, CPA. Ashraph Abdulkarim amesema uwepo wa huduma za uchunguzi na matibabu sokoni hapo ni mwendelezo wa kuhakikisha kuwa huduma zote za msingi zinapatikana katika eneo moja na kuwapunguzia wananchi usumbufu wa kutafuta huduma hizo nje ya soko hilo.
“Kama mnavyoelewa hili ni soko la kimataifa ambapo inatakiwa ukifika Kariakoo kila kitu kifanyike hapa hapa, utapata bidhaa unazozihitaji, utapata huduma za matibabu, utapata huduma za kifedha, kuna eneo la kuegesha magari hivyo unaweza kuja na gari lako na kuliegesha katika mazingira salama” amenainisha CPA. Abdulkarim
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini JKCI, Dkt. Hassan Mahamoud Mshinda amesema taasisi hiyo imeendelea kusogeza huduma karibu na wananchi na kuongeza kuwa kliniki hiyo inakuwa ya sita ukijumlisha kliniki zingine ambazo zimeanzishwa katika maeneo mbalimbali nchini.
Naye, Mkurugenzi Mtendaji JKCI, Dkt. Peter Kisenge amesema kliniki hiyo imegharimu takribani bilioni moja na itakuwa na huduma za kisasa ikiwemo matumizi ya teknolojia ya akili unde, maabara ya kisasa ambayo ni ya pekee hapa nchini na kuongeza kuwa itatoa huduma bure kwa muda wa wiki moja.
Copyright ©2024 Shirika la Masoko ya Kariakoo . All rights reserved.